Tuesday, March 4, 2014

1:27 AM

HII nayo ni kali na haijawahi kutokea. Wakazi wawili wa Vingunguti kwa Simba Mbili jijini Dar akiwemo mwenye nyumba wamekimbizwa hospitalini na polisi baada ya kunyweshwa dawa na mganga wa kienyeji waliyemleta ili azindike nyumba yao.
Tukio hilo lilitokea wiki iliyopita Vingunguti nyumbani kwa Zaina Athumani,70, ambaye ndiye mwenye nyumba aliyeleta mganga huyo ili azindike nyumba yake, mwingine aliyepatwa na tatizo hilo ni mpangaji wake aliyejulikana kwa jina la Haruna Ally.
Vyanzo vyetu vya habari vinadai kwamba Bi mkubwa Zaina alifikia hatua ya kumuita mganga huyo kutokana na kile alichodai kuwa  nyumba yake haina kinga ya aina yoyote hivyo wachawi kufanya vituko vyao usiku na sauti za ajabu kusikika hivyo kushindwa kupata usingizi.
Imeelezwa kuwa baada ya wapangaji kuingiwa na wasiwasi na sauti hizo walimuomba mama mwenye nyumba atafute mganga naye aliamua kumleta ili kuwafukuza watu waliokuwa wakipiga kelele usiku bila kuonekana.
Taarifa zaidi zilidai kwamba baada ya mganga huyo kufika nyumbani hapo alitoa vitu mbalimbali vya ajabu katika nyumba hiyo kisha kuwanywesha dawa watu zaidi ya 20 lakini mwenye nyumba na mpangaji wake mmoja walizidiwa wakadondoka chini na kuzimia ndipo mganga akaingia mitini.
Imeelezwa kuwa baada ya wapangaji kumuona mwenye nyumba ulimi umetoka nje waliangua kilio wakijua kuwa atakata roho, hata hivyo walipiga simu polisi na kuwaeleza mkasa huo.
Polisi walifika mara moja na kuwachukua wagonjwa hao na kuwakimbiza Hospitali ya Amana kwa matibabu lakini mganga akawa amekwishatoweka.
Mwandishi wa habari hizi alifika nyumbani kwa Bi mkubwa Zaina juzi na kumkuta akiwa ameshatoka Amana huku Haruna akiwa bado anaendelea na matibabu. Alipoulizwa juu ya sakata hilo alisema: “Nilikuwa na nia nzuri tu lakini nashindwa kujua kwa nini mimi ndiyo mambo yamenigeukia.
Bado najisikia vibaya kwani mwili unauma,” alisema bi mkubwa huyo, hata hivyo alidai hajui anakoishi mganga huyo kwa sababu alimpata barabarani.

0 comments:

Post a Comment