Tuesday, March 4, 2014

9:57 AM

MWANAFUNZI wa darasa la kwanza Shule ya Msingi Jangwani, Manispaa ya Sumbawanga amechomwa moto mikono yake miwili, kutokana na tuhuma za kudokoa njegere zilizokuwa zikichemka jikoni.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Jacob Mwaruanda amethibitisha mkasa huo aliouita ni wa kikatili huku akimtaja mtuhumiwa kuwa ni Anifa Lunyerere (18), mkazi wa Kitongoji cha Bangwe, Manispaa ya Sumbawanga.
Kamanda Mwaruanda alisema Lunyerere alimchoma mikono mtoto huyo (jina limehifadhiwa) wiki iliyopita katika kitongoji hicho cha Bangwe saa sita mchana.
Kwa mujibu wa Kamanda Mwaruanda, mtoto huyo alipohojiwa alidai alifikia uamuzi huo wa kudokoa njegere baada ya kuzidiwa na njaa, kwani alikuwa ametoka shuleni ambako alikuwa hajala chochote.
“Mtoto huyu alieleza kuwa wifi yake huyo amekuwa na tabia ya kumfanyia vitendo vya kikatili mara kwa mara kama vile kumng’ata mgongoni hata kama hajakosea kitu chochote,” alidai Kamanda Mwaruanda.
Mtuhumiwa huyo anashikiliwa Polisi kwa mahojiano na anatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote baada ya uchunguzi wa awali wa shauri lake kukamilika.
CREDIT: HABARI LEO

0 comments:

Post a Comment