Tuesday, March 4, 2014

10:16 AM


Ni takriban miaka 10 sasa tangu kuanzishwa kwa shule za kata hapa nchini kupitia mpango kabambe uitwao “Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES). Msisitizo mkubwa uliwekwa na Serikali kuhakikisha majengo yanajengwa hata kama hakuna mwanafunzi.
Kubwa zaidi ilikuwa ni kampeni ya kuhamasisha jamii pana kuzipokea shule hizo na kuamini kuwa ndiyo mkombozi wa wanyonge. Yaani hakuna haja ya kupeleka mtoto nje ya vijiji au kata zao, kwa kuwa shule za kata zinatosha kuwakomboa. Kwa Watanzania wengi hasa wale wa maeneo ya vijijini, uamuzi huu ulikuwa ni pambazuko jema.
Hata hivyo, watafiti na wapenda maendeleo walikosoa mapema ujenzi wa pupa wa shule za kata bila ya kuwepo kwa mkakati maalumu wa kuziwezesha kuwa na manufaa yanayotarajiwa. Watafiti na wanaharakati hawakueleweka machoni pa Serikali na baadhi ya wana jamii. Walionekana kama wahaini ama wapinga maendeleo.
Hoja kubwa kwa watawala ilikuwa ni kwamba shule hizo zipewe muda na kwamba baada ya miaka michache kila kitu kitakamilika na elimu itaboreka na Watanzania watanufaika. Kweli tukazipatia muda wa kutosha sasa ni miaka 10. Ubora wa elimu kwenye shule hizo unasikitisha.
Mwaka 2010 wanafunzi waliopata daraja sifuri na daraja la nne walikuwa asilimia 88. Mwaka 2011 walikuwa asilimia 90.2. Mwaka 2012 wakafeli asilimia 87 huku waliopata daraja sifuri wakiongezeka hadi asilimia 60.
Mwaka 2013 katika matokeo yaliyotoka hivi karibuni, waliopata sifuri na daraja la nne ni asilimia 80. Waliopata sifuri pekee ni asilimia 42. Kwa uchambuzi wa kina kama kusingepangwa madaraja kwa mfumo mpya, sifuri zingeongezeka hadi asilimia 70.
Baadhi ya shule tangu kuanzishwa kwake hazijawahi kushuhudia mwanafunzi hata mmoja akipata daraja la kwanza au la pili. Na baadhi hazijawahi kushuhudia mwanafunzi hata mmoja akipata daraja la tatu.
Kinachoshangaza hata shule zilizonadiwa kwa majina ya viongozi hazipewi msaada wowote hata wa hamasa na viongozi hao. Watoto wanaendelea kukusanya ziro kila mwaka.
Mfano ni shule kama Sekondari ya Lowasa, ambayo wanafunzi waliopata sifuri ni wanafunzi 71 kati ya wanafunzi 179, waliobahatika kupata daraja la kwanza ni 2 tu. Katika Sekondari ya Yusufu Makamba, waliopata ziro ni 112 kati ya wanafunzi 310, hakuna hata mmoja aliyepata daraja la kwanza japo shule hii iko jijini Dar es Salaam kwenye kila kitu.
Shule ya Sekondari ya Anna Mkapa kulikuwa na ziro 72 kati ya wanafunzi 192. Waliopata daraja la kwanza ni wawili tu. Pius Msekwa, sifuri ni 42 kati ya wanafunzi 124, hakuna hata mmoja aliyepata daraja la kwanza.
Sekondari ya Jakaya Kikwete, sifuri zilikuwa 43 kati ya wanafunzi 115, daraja la kwanza ni wawili tu. Sekondari ya John Malecelea ziro 15 kati ya wanafunzi 28, hakuna daraja la kwanza.
Hizi ndizo shule zenye majina ya vigogo. Hali inatisha. Tuendelee kuzipa muda hadi lini? Hali inadorora kila kukicha. Baadhi zilianza na walimu kadhaa sasa hazina walimu, na waliopo wamekata tamaa; hawajitumi kabisa.

Miaka 10 ni mingi. Kama kweli kuna nia ya kuboresha elimu hasa za mikoa masikini iliyotengwa tangu historia tungeona maendeleo. Ziko shule binafsi zinazoanzishwa ndani ya miaka miwili shule na mafanikio yanakuwa makubwa kitaifa.
Nikumbushe tu kuwa wanafunzi wanaopata sifuri katika shule za kata siyo kwamba hawana akili. Mfumo umewafelisha hata kabla hawajaanza shule. Nani asiyejua shule nyingi za kata zina upungufu mkubwa wa walimu? Baadhi ya shule zina walimu wawili tu au mmoja.
Isitoshe, shule nyingi za kata zinapokea watoto kutoka shule za msingi za Serikali ambazo wanafunzi wanafundishwa kwa Kiswahili masomo yote. Lakini, wanapoingia sekondari wanakutana na lugha ngeni na kutungiwa mitihani kwa lugha hiyo.
Wanatungiwa mitihani kwa lugha wasiyoielewa wao wala walimu wao, huku wakishindanishwa na wenzao waliosoma kwa lugha hiyo tangu chekechea.
Hakuna kiongozi asiyejua haya ndiyo maana huwezi kukuta mtoto wa kiongozi anasoma shule ya kata, japo wanazipigia debe shule hizo kwenye majukwaa.
Kwa bahati mbaya watawala wanasahau kuwa asilimia tano ya wasomi wanaofaulu vizuri hawawezi kubeba asilimia 95 ya watu wasiosoma.
Tunajidanganya. Maendeleo ya nchi huendelezwa na jamii kubwa yenye nguvu ya kuzalisha kutokana na kuwa na maarifa.
Wachache hata wakisoma vipi hawawezi kubeba wanajamii wengi. Watashika vyeo ofisini, watakuwa watawala wanyonyaji bila kuwa na ubunifu wala uzalishaji wowote.
Narudia kusema: Wanyonge Watashinda! Nguvu ya haki na utu kamwe haishindwi na fikra za uzandiki na udhalimu. Historia inathibitisha kuwa dhuluma ina uhai mfupi, huzaa fedheha ya milele na matunda ya haki hudumu na kutamalaki daima. Yanakuja!

MWANANCHI

0 comments:

Post a Comment