Tuesday, March 4, 2014

11:59 PM
 KANISA Katoliki limekanusha taarifa iliyotolewa na vyombo vya habari kuwa msimamo wa kanisa hilo ni kuwepo kwa serikali tatu katika katiba mpya.
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, amesema taarifa hiyo si sahihi bali ilitolewa na Tume ya Haki ya Baraza la Maaskofu pasipo kumshirikisha.
“Wao kama Watanzania wanayo haki ya kutoa maoni, hivyo si kosa wakiwa kama Watanzania maoni yao kuwa ni kuwepo serikali tatu, ilichokosea tume hiyo ni kusema kwamba huo ni msimamo wa Kanisa Katoliki jambo ambalo si kweli,” alisema.



Pengo alisema anakanusha vikali taaifa hiyo iliyotolewa juzi na vyombo mbalimbali vya habari hususan magazeti na kuwa Kanisa Katoliki lina wajibu wa kutoa msimamo wake katika mambo mawili tu yanayohusu imani na maadili.
“Kwa mfano ikitokea hoja kwamba kuwepo na vipengele kwenye katiba vinavyosema hakuna Mungu, kuwepo kwa ndoa za jinsia moja au kuhalalisha utoaji mimba hapo kanisa lina haki ya kusimama na kutoa msimamo wake kwani masuala hayo yanagusa  imani na maadili,”alisema.


Aliongeza kuwa anatumia nafasi hiyo katika mkutano na waandishi wa habari kutoa msimamo wake kama Mtanzania wa kawaida  kuwa mapendekezo yake ni kuendelea kuwepo kwa serikali mbili yaani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Mapinduzi ya Zanzibar.


“Kama kuna dosari zozote zilizojitokeza wakati wa kuasisi Muungano zinazotishia umoja wa kitaifa ni heri zikarekebishwa ili uendelee mfumo wa serikali mbili kwani serikali tatu ni mzigo,” alisema.
Vilevile alitoa maoni kuhusu suala la kura katika bunge la katiba na kusema kwamba anaunga mkono kutumika kwa kura ya siri kwani ni ya uhakika zaidi kuliko ya wazi  ambayo wengine wanaweza kufuata mkumbo ili mradi wasionekane wasaliti.


Mwishoni mwa wiki iliyopita, Tume ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) ilitoa tamko ikitaka Bunge Maalumu la Katiba kuepuka kukashifu mapendekezo ya muundo wa serikali tatu.

 

0 comments:

Post a Comment