Thursday, December 5, 2013

3:04 AM

Polisi mkoani Arusha imekamilisha uchunguzi wake kuhusiana na kuungua kwa Ofisi za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kusema wanachama wa chama hicho ndio waliohusika. 
 
Hata hivyo, Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema amepinga kauli hiyo na kulipa jeshi hilo siku nne kuwakamata na kuwahoji watuhumiwa watano baada ya kulipatia majina hayo akidai kuwa ndio wanaohusika na uchomaji moto ofisi za chama hicho.
 
“Tumewapatia polisi majina... tunaamini walihusika moja kwa moja la sivyo, chama kitatumia vijana wetu wa Red Brigade kuwakamata na kuwafikisha polisi,” Lema aliwaambia waandishi wa habari jana.
 
Ofisi za Chadema zilizoko katika eneo la Ngarenaro, zilinusurika kuteketea kwa moto juzi baada ya watu wasiojulikana kuwasha moto katika moja ya vyumba vyake.
 
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Japhet Lusinga alisema:
 
“Katika uchunguzi wetu, tumebaini kuwa hakuna mahali palipovunjwa kutoka nje ya uzio na kuruhusu watu kuingia ndani... tumegundua kuna tundu dogo darini eneo la kuelekea bafuni la upana wa futi moja na nusu kiasi haliwezi kuruhusu mtu kupita.
 
“Tumejiridhisha kuwa hakuna mtu anayeweza kupita hapo na ndani tulikuta majivu na baadhi ya vitu vilivyoungua na vifaa vingine.”
 
Lema akiwa na Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Arusha, Ephata Nanyaro alisema: “Tumebaini polisi wanataka kulifanya jambo hili kama la siasa ndiyo sababu juzi badala ya kuanza kuchunguza waliohusika, waliwakamata Mtunza Ofisi na mlinzi wetu na kuwalaza rumande hadi leo (jana) asubuhi kwa madai eti wanawahoji.
 
“Hatukubaliani na taarifa yao, hii ni siasa. Kulitokea mauaji ya bomu, wakasema Chadema wamejilipua, leo ofisi imechomwa wanasema Chadema wenyewe, hili hatukubali, “ alisema.
 
Msajili alaani
Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi amelaani tukio la kuchomwa moto ofisi hizo za Chadema na kusisitiza kuwa wananchi hususan wanasiasa wasiwe wepesi kuingiza hisia kwenye makosa ya kijinai.
 
Alisema kuwa tukio hilo linapaswa kukemewa kwa hali yoyote ile kwa kuwa linavuruga na kuhatarisha amani ya nchi.

0 comments:

Post a Comment