Monday, December 2, 2013

4:18 AM
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimemuomba Rais Jakaya Kikwete kuvunja Baraza la Mawaziri kisha awaondoe wanaotajwa kuwa mizigo.



Akizungumza Dar es Salaam jana, wakati wa uzinduzi wa Rasimu ya Sera ya Chadema ya Mabadiliko ya Tabianchi, Mkurugenzi wa Habari na Uenezi, John Mnyika, alisema Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni itakwenda kuwabana mawaziri hao katika mkutano wa Bunge utakaoanza kesho.

Alisema mawaziri hao ambao ni wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamekuwa wakitajwa na wabunge wenzao katika mikutano ya ndani na katika mikutano ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, lakini hawachukuliwi hatua.

“Kama wabunge wa CCM, Kinana na Nape hawakuwa wanafiki, basi wabunge wao wawe wa kwanza kuchukua hatua kabla mawaziri vivuli hatujawashughulikia.

“CCM wamekuwa wakiwazungumzia mawaziri mizigo na Rais Kikwete hajawahi kuwashughulikia, wanajaribu kuwakwepesha kwamba watakwenda kujadiliwa na Kamati Kuu yao, kama Kinana hakuwaelekeza wabunge wake sisi tutaifanya kazi hiyo.

“Sisi tunawaambia Kinana na Nape, wasome Katiba ya nchi, Bunge ndilo lenye uwezo wa kuwawajibisha wabunge, sasa Bunge liwawajibishe au rais aliyewateua avunje Baraza la Mawaziri.

“Kati ya wanaolalamikiwa amekuwa akisemwa Waziri wa Mifugo, lakini wanaogopa kumsema Waziri wa Kilimo, sasa waziri wetu kivuli atakwenda kumbana,” alisema Mnyika.

Akizungumzia rasimu yao, alisema majanga mengi ya asili yakiwamo ukame, njaa na mafuriko chanzo chake ni mabadiliko ya tabianchi.

Alisema Serikali haijaweza kushughulikia matatizo ya mabadiliko ya tabianchi, kutokana na sheria ya mazingira ya mwaka 2004 kupitwa na wakati.

“Asilimia 70 ya majanga ya asili chanzo chake ni mabadiliko ya tabianchi, kama hatutachukua hatua mapema uhai wa Mlima Kilimanjaro utakuwa shakani kutokana na kupungua kwa theluji.

“Lakini pia chanzo cha mgao wa umeme tunaambiwa ni kupungua kwa kina cha maji, hii pia chanzo chake ni mabadiliko ya tabianchi.

“Kupitia rasimu hii, tunaomba mawazo na maoni ya wananchi na kisha tutafanya utekelezaji wa kuibana Serikali juu ya sera hii,” alisema Mnyika.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) na Katibu Mkuu wa kwanza wa Chama cha Wafanyakazi Madaktari na Wafamasia (TMDPWU), Dk. Rodrick Kabangila, amejiuzulu nyadhifa hizo baada ya kuchaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Chadema, Kanda ya Ziwa Magharibi.

Alisema amechukua uamuzi huo kuondoa mgongano wa kimaslahi kati ya vyama anavyoviongoza, madaktari na Chadema.

“Pamoja na mambo mazuri niliyohusika katika kuongoza madaktari na kuwa na moyo wa kuendelea kufanya hivyo, bado kuna mambo mengi hayaendi vizuri ambayo ni ya kimfumo katika Serikali ya CCM ambayo yanaendelea kudidimiza huduma za afya.

Mifano mizuri katika hili ni urasimu usio na maana katika usambazaji wa dawa na vifaa tiba, kutojali wataalamu, ufisadi na uzembe kuanzia wizarani, taasisi zake kama bohari ya dawa hadi katika vituo vya afya,” alisema Dk. Kabangila.


TOA MAONI YAKO KATIKA SEHEMU YA COMMENTS 

0 comments:

Post a Comment