Thursday, December 5, 2013

6:29 AM
 Mama mzazi wa Zitto Zuberi Kabwe.
MAMA mzazi wa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, Shida Salum amenusurika kifo baada ya gari alilokuwa akisafiria kutoka Dar es Salaam kuelekea mkoani Lindi kupata ajali mbaya.
Habari ambazo zililifikia  jana jioni muda mfupi tu baada ya kutokea kwa ajali hiyo, zilieleza kuwa chanzo chake ni kupasuka kwa tairi la nyuma wakati gari likiwa kwenye mwendo mkali.
Kwa mujibu wa habari hizo, ingawa Mama Zitto hajaumia lakini gari hilo liliharibika vibaya kutokana na kubiringika mara kadhaa kabla ya kuangukia porini.Mama Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Walemavu (CHAMATA), alikuwa akielekea kwenye ziara ya kikazi mkoani Lindi na alipata ajali hiyo muda mfupi baada ya kutoka kwenye maadhimisho ya siku ya watu wenye ulemavu yaliyofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja, ambapo Rais Jakaya Kikwete alikuwa mgeni rasmi.

Akizungumza kupitia simu yake ya kiganjani na RAI Jumatano, Mama Zitto alisema anamshukuru Mungu kwa kuwa hajaumia.

Alisema ajali hiyo ilitokea katika eneo la Nguruku Wilaya ya Mkuranga na kwamba hakuna aliyeumia lakini gari limeharibika vibaya.

Namshukuru Mungu kwa kunusurika na ajali hii ambayo hata hivyo nilimuona dereva akijitahidi kutuokoa, lakini ikashindikana.

Nashukuru kwani wanangu wamenitumia gari lingine na inanibidi niendelee na safari kwani kesho asubuhi (leo) ninaanza mkutano,” alisema Mama Zitto.
Source: Mtanzania

0 comments:

Post a Comment