Tuesday, December 3, 2013

1:48 PM

Mbunge wa Nzega, Dk Khamis Kigwangalla (CCM) amesema anajipanga upya kuhakikisha hoja yake ya kutaka kumng’oa madarakani Spika wa Bunge, Anne Makinda inarejea tena bungeni licha ya kutupwa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.
 

Dk Kigwangalla alisema jana kwamba, hakuridhika na majibu ya kamati hiyo kuhusu sababu za kuitupa hoja yake, kwani wakati akiitoa alieleza sababu za kisheria na kanuni zilizokiukwa na Makinda, hivyo alitaka kuelezwa sababu siyo kukataliwa pekee.

Katika ufafanuzi wake jana, Dk Kigwangalla alisema: “Kanuni ya Bunge ya 137 Ibara ya kwanza inaeleza utaratibu wa mtoa hoja kuiwasilisha kwa maandishi kwa Katibu wa Bunge, nimeletewa barua kutoka ofisi ya Bunge ambayo haijaeleza sababu za hoja yangu kukataliwa.”

“Nimeipata barua ya kamati hiyo. Katika hoja yangu nilichambua ukiukwaji uliofanywa na Spika Makinda kwa kutumia kanuni na sheria zilizopo, nilitarajia hoja ingeletwa bungeni lakini wameikataa.”

Dk Kigwangalla alisema hivi sasa anapitia sheria na kanuni za Bunge ili kuona uamuzi atakaochukua baada ya hoja yake kukataliwa.

“Ngoja napitia kanuni na sheria za Bunge, nitajua cha kufanya kuhusu hili katika vikao vinavyoanza kesho (leo),” alisema mbunge huyo.

Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah alisema taarifa kuhusu kukataliwa kwa hoja hiyo inaweza kutolewa rasmi iwapo kamati itaona umuhimu wa kufanya hivyo.

“Kama kamati ingeridhika kwamba kuna hoja muhimu, ingependekeza suala hilo kupelekwa bungeni, lakini ilipofanya uchambuzi haikuona umuhimu huo, sisi tulishamwarifu mhusika,” alisema Dk Kashililah.

Miongoni mwa madai ya Dk Kigwangalla katika hoja hiyo aliyotoa katika mkutano wa Bunge uliopita, ni kwamba Spika amekuwa akikiuka kanuni za Bunge kwa kuzuia mijadala ya dharura na kutokutoa nafasi kwa hoja za wabunge kama kanuni zinavyoelekeza.

Madai mengine ni kuzuia kwa mabavu majedwali ya mabadiliko ya sheria kwenye kamati ya bajeti, kuvunja masharti ya kanuni ya 48 inayotoa maelekezo ya namna ya kuwasilisha na kujadili jambo la dharura na kutumia madaraka vibaya kwa kuvunja masharti ya Sheria ya The National Assembly (Adminishation) Act (Cap.115) ya mwaka 2008.

Suala jingine ni kumteua Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, tofauti na kanuni zinazotaja wenyeviti kuchaguliwa na wajumbe wa kamati.
Pia, wanadaiwa kulipwa posho ya Sh430,000 wakati kamati nyingine wamekuwa wakipewa Sh130,000.

0 comments:

Post a Comment