Sunday, March 2, 2014

2:47 AM

Kwa kawaida uvaaji wa mavazi hutegemea hali ya hewa au majira ya husika ya mwaka. Ni muhimu kuzingatia majira ili kuepuka shida au kukosa raha kwa kuchagua vazi lisilo sahihi.
Majira ya joto watu wengi hupata shida ya kuchagua mavazi, kwani kipindi hicho huwa ni vigumu kwao kuvaa vizuri waendapo kazini au kutoka kwa ajili biashara au shughuli zao nyingine.
Hata hivyo, kabla hujachagua kuvaa nguo, hata kama ofisi yako ina utaratibu wa mavazi rasmi ya wakati wa joto, kumbuka mavazi yako yana nafasi kubwa kwa mwonekano wako na hali ya joto haiwezi kukubadilisha. Kumbuka kuwa huna sababu ya kuvaa nguo zisizofaa ili kuepuka joto. Siku zote jiamini na hakikisha unapambana na joto ukilenga kuonekana nadhifu.
Ufuatao ni mwongozo, ambao ukiufuata utakuwezesha kufikia malengo yako ya kuonekana nadhifu kipindi cha joto, kwani ukifanikiwa kuufuata vizuri, utaonekana mwenye kujua maana halisi ya mitindo.
Unachotakiwa kufanya
* Vaa nguo zenye tabaka mbili, hii itakurahisishia kubadilisha kuendana na mabadiliko ya hali ya hewa. Hapa unaweza kuvaa blauzi yenye mikono mifupi au ‘top’ na jaketi jepesi ‘blazer’ au koti. Hii itakurahisishia kuweza kulivua jaketi hilo au koti ikiwa utasikia joto.
unaweza kuvua jaketi au koti lako na kubakia na blauzi au ‘top’.
* Jaribu kuvaa sketi badala ya suruali, hata kama unapendelea kuvaa suruali, kwani sketi huruhusu hewa kuzunguka katikati ya mapaja na kuondoa hali ya joto.
* Ili kuepusha usumbufu, hakikisha nywele zako hazikugusi, hivyo ni vizuri ukazibana kwa mtindo utakaofanya zisiguse shingo yako. Unaweza kuzikusanya katikati na kuzibana au kuzisuka. Staili hizi zitafanya nywele zako zisikuguse shingo.
* Paka vipodozi vilivyo angavu, hasa ukiwa nje kwenye joto kali. Joto kali na vipodozi vingi haviendani. Joto husababisha vipodozi kuyeyuka na kuondoka, pia husababisha vitundu vya hewa kuziba na ngozi kupasuka.
*Jipake manukato mazuri yanayoendana na majira ya joto. Manukato yenye harufu kali hunukia vibaya kwenye joto.
* Mavazi huendana na vitu vingine kama pochi, viatu, mkanda, hata herein au mkufu. Unashauriwa kubeba pochi na kuvaa viatu vyenye rangi angavu.
Usichotakiwa kufanya
* Usivae ‘top’ isiyo na mikono kazini, hata kama una mikono mizuri.
* Usivae kaptula au sketi fupi, labda kama ni sare ya ofisi.
* Usivae viatu vya wazi. Vaa viatu vya kawaida, hasa vinavyofunika vidole .
* Epuka kuvaa rangi zinazowaka sana, unaweza kuvaa nguo za rangi mbalimbali, lakini zisiwe rangi zinazowaka sana. Kumbuka ; unataka watu wakuangalie wewe na siyo rangi ya nguo yako.
Usikubali kuharibu mwonekano wako kwa sababu ya mabadiliko ya hewa, hakikisha kabati lako lina nguo zinazokwenda na halijoto, wakati huo huo mwonekano wako unaendelea kufanana na taaluma yako.
Imeandaliwa na Maimuna Kubegeya
Baruapepe :maikube@yahoo.co.uk

Tupe Maoni yako hapo chini

0 comments:

Post a Comment